IQNA

Mkutano wa Umoja wa Kiislamu kufunguliwa na Rais Rouhani

19:51 - December 26, 2015
Habari ID: 3469673
Rais Hassan Rouhani wa Iran anatazamiwa kutoa hotuba katika ufunguzi wa mkutano wa 29 kimataifa wa Umoja wa Kiislamu Jumapili hapa mjini Tehran.

Manouchehr Mottaki Msemaji wa Jumuiya ya Kimataifa ya Kukurubisha Madhehebu za Kiislamu inayoandaa mkutano huo amewambia waandishi habari kuwa mbali na hotuba ya Rais Rouhani kikao hicho cha ufunguzi pia kitahutubiwa na wanazuoni na maafisa wa ngazi za juu wa nchi za Kiislamu. Amesema mkutano huo ambao unafanyika kwa munasaba wa Mawlid ya Bwana Mtume Muhammad SAW na  Wiki ya Umoja wa Kiislamu utahudhuriwa na wageni zaidi ya 300 kutoka nchi 70 duniani. Ameongeza kuwa mkutano wa mwaka huu utajadili mada kuu ya "Migogoro ya Sasa Katika Ulimwengu wa Kiislamu" na kwamba kongamano hilo. Mottaki ameongeza kuwa mkutano wa mwaka huu utakuwa na kamati 12 ambazo zitajadili masuala kama vile sayansi na teknolojia, vyuo vikuu, utatuzi wa migogoro, tathmini ya migogoro katika ulimwengu wa Kiislamu na njia za kujikwamua, muqawama, familia, wanawake, biashara na vijana. Kwingineko Mottaki ameashiria hali ya Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria Sheikh Ibrahim Zakzaky anayeshikiliwa na jeshi la nchi hiyo na kusema: "Jumuiya ya Kimataifa ya Kukurubisha Madhebu za Kiislamu ina wasi wasi mkubwa kuhusu hali ya kiafya ya Sheikh Zakzaki. Amesema Jumuiya hiyo inaitaka serikali ya Nigeria isitishe ukandamizwaji wa Waislamu nchini humo na kuchukua hatua dhidi ya waliotenda jinai dhidi ya Waislamu katika mji wa Zaria.

3469473

Kishikizo: iran rouhani umoja kiislamu
captcha