IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Uislamu utumike kukabiliana na fitina za wakufurishaji

22:12 - February 23, 2016
Habari ID: 3470158
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, kuimarisha harakati za Kiislamu ndiyo njia mwafaka ya kukabiliana na fitina za makundi ya wakufurishaji katika mataifa mbalimbali.
Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ameyasema hayo leo alasiri mjini Tehran katika mazungumzo yake na Ilham Aliyev Rais wa Jamhuri ya Azerbaijan.
Katika kikao hicho, Kiongozi Muadhamu w amesema uhusiano wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Jamhuri ya Azerbaijan ni mzuri.

Huku akiashiria uhusiano mzuri wa kisiasa na nukta nyingi za pamoja baina ya Iran na Azerbaijan hasa nukta za pamoja za kidini na kimadhehebu baina ya mataifa mawili, amesema kuhimizwa mafundisho ya Kiislamu na kuheshimu dhihirisho na nembo za kidini ni mambo ambayo yatavutia umma na kuwafanya wananchi wasaidie katika kukabiliana na vitisho. Ayatullah Khamenei amesema mtazamo wa Jamhuri ya Kiislamu kwa watu wa Azerbaijan ni kwa msingi wa udugu ambao ni muhimu zaidi ya masuala ya urafiki na ujirani. Ameongeza kuwa, uthabiti wa kisiasa, usalama, utulivu na maisha bora ya wananchi wa Azerbaijan ni masuala muhimu sana kwa Iran. Amesema kutokana na maelewano ya karibu ya mataifa mawili, kunapaswa kuzidisha ushirikiano wa kiuchumi baina ya nchi mbili.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria pia nukta za pamoja za kimadhehebu baina ya watu wa Iran na Jamhuri ya Azerbaijan na kusisitiza kuwa: "Itikadi za Kiislamu na madhehebu ya Kishia miongoni mwa watu wa Azerbaijan ni rasilimali yenye thamani na kadiri serikali itakavyoheshimu madhihirisho na itikadi za kidini na kuyakaribisha, basi wananchi nao watazidisha uungaji mkono wao kwa serikali sambaba na kukabiliana na uadui wa baadhi ya madola makubwa ya kibeberu."  Aidha amekumbusha kuwa Jamhuri ya Azerbaijan imekita mizizi kwa matazamo wa kidini na kwamba ni kitovu cha baadhi ya maulamaa wakubwa wa Kiislamu. Amesema watu wa Azerbaijan ni watu wenye uelewa na makini na kwa hivyo msaada wa serikali katika harakati za kidini ni jambo litakalokuwa na taathira kubwa. Ayatullah Khamenei ameunga mkono tamko la Rais wa Azerbaijan kuhusu kuwepo chimbuko moja la aghlabu ya vitisho dhidi ya nchi mbili hizi na kuongeza kuwa, kueneza mafundisho ya Kiislamu na Kishia ni jambo ambalo litapelekea kuwepo msaada na nusura ya Mwenyezi Mungu na dua za Maimamu watoharifu mkabala wa matatizo na vitisho.

3477920


captcha