IQNA

Zarif: Taifa la Iran halitasalimu amr mbele ya mashinikizo ya utawala wa Marekani

13:55 - July 02, 2019
Habari ID: 3472030
TEHRAN (IQNA) - Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema taifa la Iran katu halitasalimu amri mbele ya mashinikizo ya Marekani.

Mohammad Javad Zarif aliysema hayo Jumatatu mjini Tehran katika hafla ya kuadhimisha Siku ya Kitaifa ya Viwanda na Madini Iran na kuongeza kuwa, mashinikizo ya Marekani dhidi ya Iran si dalili ya nguvu na uwezo mkubwa wa utawala huo wa  kibeberu na wala si ishara kuwa Iran ni taifa dhaifu.

Amesema Jamhuri ya Kiislamu inafanya kazi na kushirikiana na mataifa mengine ya dunia ili kuipa funzo Marekani juu ya namna ya kuamiliana na kuzungumza kwa lugha ya heshima na isiyo ya vitisho na taifa hili.

Zarif amesema mwaka uliopita Marekani ilifanya juu chini na kuchukua hatua ya mbali zaidi ya kulirai mara nne Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kufanya kikao cha kutafuta eti muafaka dhidi ya Iran, lakini ombi lao hilo liligonga mwamba.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kwa kusimama kidete na kutotetereshwa na mashinikizo ya maadui, taifa hili limeweza kuimarisha izza na heshima yake katika eneo, katika hali ambayo Marekani imezidi kutengwa na kuchukiwa.

Baada ya kujiondoa katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA Mei mwaka jana, utawala wa Marekani ulianzisha tena vikwazo dhidi ya Iran ikiwa ni pamoja na kuzuia uuzaji wa mafuta ghafi ya petroli ya Iran nje ya nchi. Hatua hiyo ya Marekani kukiuka JCPOA na kuiwekea Iran vikwazo inaendelea kulaaniwa kimataifa.

3823496

captcha