IQNA

Netanyahu na mkuu wa Mossad walitembelea Saudia kwa siri

20:22 - November 23, 2020
Habari ID: 3473385
Waziri Mkuu wa utawala huo Benjamini Netanyahu na baadhi ya maafisa wa Shirika la Ujasusi la Israel (MOSSAD) wamefanya ziara ya siri kwa wakati mmoja na Mike Pompeo Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani.

Duru za habari zinadokeza kuwa kuwa, katika safari yake hiyo ya siri nchini Saudi Arabia Benjamin Netanyahu amekutana na kufanya mazungumzo na Muhammad bin Salman mrithi wa kiti cha ufalme wa Saudi Arabia. Gazeti la Kizayuni la Haaretz limedokeza kuwa, katika safari hiyo ya siri nchini Saudia, Yossi Cohen, mkuu wa shirika la  kijasusi la Israel Mossad aliandamana  Netanyahu ambapo walishiriki katika mazungumzo yaliyomjumuisha Muhammad bin Salman na Mike Pompeo katika mkoa wa Tabuk nchini humo. 

Imearifiiwa kuwa, katika hali ambayo  safari hiyo ya Waziri Mkuu wa Israel imesajiliwa kwenye tovuti ya kimataifa ya kufuatilia nyendo za ndege (Flight Tracking) lakini ofisi ya Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni imekataa kutoa maelezo yoyote kuhusu ziara hiyo. Netanyahu amefanya ziara hiyo nchini Saudi Arabia huku Mike Pompeo Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani akiwa katika ziara ya kuzitembelea nchi kadhaa za eneo hili. 

Inaonekana kuwa mazungumzo ya viongozi hao wa Israel, Saudia na Marekani yanajiri katika juhudi za rais wa Marekani, Donalda Trump za kuendeleza mchakato wa kuanzisha uhusiano rasmi kati ya utawala wa Kizayuni na baadhi ya tawala za Kiarabu za eneo hili. 

Ikumbukwe kuwa Tarehe 15 Septemba mwaka huu, Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Bahrain walitia saini makubaliano ya kutangaza uhusiano wa kawaida baina ya nchi zao na utawala ghasibu wa Israel.

Sherehe hizo zilizofanyika katika Ikulu ya Marekani, White House, zilihudhuriwa pia na rais wa Marekani, Donald Trump na Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala dhalimu wa Israel. Mwezi Oktoba pia Sudan nayo pia ilitangaza kuafikia kuanzisha uhusiano na utawala wa bandia wa Israel. Waislamu na wapigania haki kote duniani wanapinga hatua ya nchi hizo za Kiarabu kuanzisha uhusiano na Israel kwani hatua hiyo ni sawa na kusalitiwa na kupigwa jambia kwa nyuma Wapalestina.

3473204

captcha