IQNA

Waislamu wa Russia watangaza kuunga mkono ukombozi wa Palestina

19:29 - May 07, 2022
Habari ID: 3475220
TEHRAN (IQNA)- Waislamu nchini Russia wametangaza uungaji mkono jitihada za ukombozi wa taifa linalodhulumiwa la Palestina ambalo linakoloniwa na utawala haramu wa Israel.

Mkuu wa Baraza la Mamufi wa Russia Sheikh Ravil Ainuddin ametangaza himaya na uungaji mkono huo wa Waislamu wa nchi hiyo katika mazungumzo yake mjini Moscow na Moussa Abu Marzouq, mjumbe mwandamizi wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiisamu ya Palestina HAMAS.

Sheikh Ravil Ainuddin amesisitiza katika mazungumzo hayo juu ya himaya na uungaji mkono wa Waislamu wa Russia kwa wananchi wa Palestina na kubainisha kwamba, hali ya mambo kwa Wapalestina huko Quds (Jerusalem) imekuwa ngumu na kwamba, anafuatilia kwa karibu yale yanayojiri katika mji huo mtakatifu.

Mkuu wa Baraza la Mamufti Russia sambamba na kuonyesha kuwa pamoja na Wapalestina walioko Quds au Baytul-Muqaddas amesema kuwa, kama kutakuweko na uwezekano yuko tayari kutoa msaada wowote ule.

Halikadhalika kiongozi huyo wa kidini ameashiria juhudi za kidiplomasia za Russia kwa ajili ya kuipatia ufumbuzi kadhia ya Palestina na kueleza kwamba, Russia  inatambua rasmi azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linalotilia mkazo juu ya kuundwa nchi huru la Palestina yenye mamlaka kamili.

Kwa upande wake, Moussa Abu Marzouq, afisa mwandamizi wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiisamu ya Palestina HAMAS amemshukuru Sheikh Ravil Ainuddin na Waislamu wote wa Russia kwa himaya na uungaji mkono wao  kwa kadhia ya Palestina pamoja na misimamo yao thabiti kuhusiana na Palestina.

Ujumbe wa Hamas uliwasili Russia Jumatano iliyopita kwa lengo la kufanya mazungumzo na maafisa wa ngazi za juu wa Russia.

4055039

captcha