IQNA

Jinai za Israel

Askari katili wa Israel wamuua shahidi kijana Mpalestina

12:22 - June 25, 2022
Habari ID: 3475423
TEHRAN (IQNA)- Wanajeshi wa Israel wamemuua kijana wa Kipalestina wakati wa kukamatwa katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu

Kijana wa Kipalestina amefariki dunia baada ya kukamatwa na kushambuliwa na wanajeshi wa Israel kwenye viunga vya Ramallah katikati mwa Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu, kwa mujibu wa familia yake na vyombo vya habari vya Palestina.

Kijana huyo aliyetambuliwa na shirika la habari la Sama la Kiarabu kama Abdullah Muhammad Hammad mwenye umri wa miaka 16 alipigwa risasi na kujeruhiwa mapema Jumamosi wakati wanajeshi wa Israel walipojaribu kumkamata katika mji wa Silwad, ulioko kilomita 12 (maili 7.4) kaskazini mashariki mwa Ramallah. .

Hammad alipelekwa kusikojulikana akiwa katika hali mbaya, kabla ya familia yake kufahamishwa kuhusu kifo chake.

Haya yanajiri saa chache baada ya Wapalestina zaidi ya mia moja kujeruhiwa katika mapigano na jeshi la Israel katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu.

Vikosi vya Israel vilifyatua risasi za moto, risasi za mpira na gesi ya kutoa machozi dhidi ya Wapalestina waliokuwa wakifanya maandamano katika Ukingo wa Magharibi siku ya Ijumaa, ikiwa ni pamoja na katika mji wa kaskazini wa Kafr Qaddum, Qalqilya, na mji wa Beita, kusini mwa Nablus, kama sehemu ya maandamano yao ya kila siku. dhidi ya makazi haramu ya Israel, ambayo yalianza wiki za hivi karibuni.

Katika taarifa yake, Jumuiya ya Hilali Nyekundu ya Palestina (PRCS) ilisema Wapalestina wasiopungua 131 walijeruhiwa, wakiwemo tisa kwa risasi za moto, huku 117 wakikosa hewa kutokana na gesi ya kutoa machozi.

Israel inaanzisha kituo cha makazi, kinachojulikana kama Avitar, kwenye takriban mita za mraba 1,000 (futi za mraba 10,764) za ardhi inayokaliwa katika kitongoji cha mji wa Jabal Sabih, na kusababisha maandamano.

Siku ya Jumanne, mwanamume Mpalestina alikufa baada ya kuchomwa kisu na walowezi wa Kiisraeli katika kijiji cha Iskaka, katika eneo la Salfit linalokaliwa kwa mabavu na Ukingo wa Magharibi, kulingana na Wizara ya Afya ya Palestina.

Maafisa wa afya walimtaja mwathiriwa kama Ali Hassan Harb mwenye umri wa miaka 27, ambaye alifariki kutokana na jeraha mbaya la kuchomwa kifuani, shirika rasmi la habari la Palestina Wafa liliripoti.

Duru za ndani zilisema kuwa ugomvi ulizuka baada ya walowezi wa Israel kujaribu kutwaa shamba la ardhi ya kijiji cha Wapalestina kwa kuweka hema kwenye mali ya kibinafsi.

4066364

captcha