Mkutano wa kila mwaka ambao huandaliwa na Jamii ya Waislamu Marekani (MAS) na Jumuiya ya Kiislamu ya Amerika Kaskazini (ICNA) ulifanyika Disemba 27-29 ambapo ajenda kuu ya mwaka huu ilikuwa ni "Uislamu: Kukabiliana na Changamoto za Leo na Kuwekeza Kwa Ajili ya Mustakabali Bora."
Mkutano huo ulikuwa na mamia ya wazungumzaji, warsha, mazungumzo ya meza duara, maonyesho ya sanaa, filamu, soko la bidhaa mbali mbali, nk.
Lengo la mkutano huo limetajwa kuwa ni kuwaunganisha Waislamu na pia kuuarifisha Uislamu kwa wasiokuwa Waislamu ili watu wote katika jamii waishi kwa amani na maelewano.
Kati ya wazungumazaji mashuhuri katika kongamano la mwaka huu ni pamoja na Abdul Malik Mujahid, Javaid Siddiqie, Naji Nihad Awad, Siraj Wahaj Suzy Ismail, Zaynab Ansari na Karen Danielson.
Uchunguzi uliofanywa na kituo cha utafiti cha Pew nchini Marekani umeonesha kuwa, idadi ya Waislamu nchini humo itakuwa ya pili kwa ukubwa, baada ya Ukristo kufikia mwaka 2040.
Kwa mujibu wa ripoti ya kituo hicho, idadi ya Waislamu nchini humo inaongezeka kwa wastani wa watu laki moja kila mwaka. Uchunguzi wa Pew umesema idadi ya Waislamu nchini Marekani itaongezeka na kuipiku ile ya Mayahudi. Kwa mujibu wa kituo hicho, kufikia mwishoni mwa mwaka wa 2017, idadi ya Waislamu wanaoishi Marekani kihalali ilikuwa milioni 3.4. Hata hivyo takwimu za taasisi huru za Kiislamu nchini humo kama vile Baraza la Mahusiano ya Kiislamu Marekani (CAIR) zinaonyesha kuwa, kuna Waislamu kati ya milioni 6 na 8 kati ya watu wote milioni 329.