Sayyid Muhammad Sadat Nejad amesema hayo katika hotuba yake katika kikao cha 48 cha Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa ambapo amebainisha kwamba, katika kipindi cha miongo saba iliyopita Palestina imeshuhudia jinai zisizo na idadi kama mauaji ya umati, uangamizaji wa kizazi, kubadilisha muundo wa kijamii, mateso, kamatakamata na aina kwa aina ya jinai za kivita, mauaji ya kimbari na jinai dhidi ya binadamu.
Akizungumzia kuendelea jinai za utawala dhalimu wa Kizayuni wa Israel huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu, mwakilishi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika kikao cha Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa mjini Geneva Uswisi ameashirIa masaibu ya mamia ya watoto wa Kipalestina katika magereza ya kuogofya ya Israel na kukumbusha kwamba, aghalabu ya watoto hao wanashikiliwa jela kwa kosa la kuwarushia mawe wanajeshi wa Israel.
Mwanadiplomasia huyo wa Iran amebainisha kwamba, kushindwa jamii ya kimataifa kuulazimisha utawala huo ghasibu ili ushikamane na kuheshimu sheria za kimataifa yanayafanya majukumu ya Baraza la Haki za Binadamu kuwa maradufu na mazito zaidi,ambapo taasisi hiyo inapaswa kuchukua hatua za haraka na za maana kwa ajili ya kuhitimisha jinai dhidi ya wananchi madhulumu wa Palestina.
Aidha amesema kuwa, madola yanayouunga mkono utawalaa vamizi wa Israel kama Marekani, waitifaki wake wa Ulaya na Canada wanapaswa kutoa majibu kutokana na kuzuia kutekelezwa uadilifu.