Ramadhani, mwezi wa tisa katika kalenda ya Kiislamu, unatarajiwa kuanza Aprili 3, ambapo Waislamu duniani kote hufunga kula na kunywa kuanzia alfajiri hadi magharibi.
Ili kuhakikisha bidhaa zinakidhi mahitaji ya watu wengi wakati wa Ramadhani, wakuu wa Morocco wamesisitiza kwamba wanachukua hatua kuhakikisha usambazaji hautasitishwa au kuvurugwa katika mikoa yote kote Morocco.
Waziri wa Viwanda na Biashara Ryad Mezzour alihudhuria mkutano ambao Waziri wa Mambo ya Ndani Abdelouafi Laftit aliongoza kujadili ufuatiliaji wa hali ya usambazaji wa vyakula katika soko la kitaifa.
Mezzour aliwahakikishia wananchi kwamba licha ya kuongezeka kwa matumizi ya baadhi ya vyakula vya msingi wakati wa Ramadhani, usambazaji wa bidhaa hizo utaendelea bila tatizo katika mikoa yote nchini Morocco.
Mezzour alisema kuwa serikali itahakikisha kuwa bei za bidhaa hizo zinafaa, ili kulinda uwezo wa ununuzi wa wananchi pamoja na afya na usalama wa watumiaji.
Matamshi ya kutia moyo ya Morocco yalikuja huku kukiwa na ongezeko kubwa la bei za bidhaa muhimu ambazo hutumiwa kwa kawaida wakati wa Ramadhani.
Hivi majuzi wananchi walizindua heshtegi katika mitandao ya kijamii, wakitaka kusitishwa kwa ongezeko la bei za vyakula kwani hali hiyo imepelekea kupungua uwezo wao wa kununua.
Serikali ilisema kuwa ongezeko la bei linatokana na hali ya kimataifa na mzozo wa kiuchumi kote ulimwenguni.
Serikali ilisisitiza zaidi kuwa imejipanga kukabiliana na athari za hali hiyo kwa kutoa ruzuku kwa bidhaa kadhaa, ikiwa ni pamoja na unga.
3478047