Rais aliyasema hayo Jumapili alipokutana na kuzungumza na Rais Recep Tayyib Erdogan wa Uturuki pambizoni mwa kikao cha 15 cha Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiuchumi ECO huko Ashgabat, mji mkuu wa Turkmenistan.
Katika mazungumzo hayo Rais Ebrahimi ameelezea wasiwasi wake kuhusiana na uwepo wa magaidi wa Daesh katika nchi jirani ya Afghanistan na hali ya kusikitisha ya usalama wa nchi hiyo iliyoharibiwa na vita vya ndani. Amesema inasikitisha kuona kwamba magaidi hao hawahatarishi usalama wa Afghanistan pekee bali na wa nchi nyingine za eneo. Rais Ebrahim Raisi amesisitiza kwamba Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inaunga mkono kikamilifu juhudi za kubuniwa serikali kuu itakayoyajumuisha makundi yote ya Afghanistan kwa ajili ya kushirikiana katika uendeshaji wa mambo ya nchi hiyo.
Licha ya askari wa Marekani kuivamia kijeshi nchi hiyo Oktoba 2001 kwa madai ya kusaka na kuwakandamiza magaidi wa Daesh lakini hata baada ya kupita miaka 20 ya uwepo wake katika nchi hiyo hakuna lolote la maana ililofanya katika kuidhaminia Afghanistan usalama wake bali karibuni ililazimika kuharakisha kuondoa askari wake nchini humo baada ya kushindwa kufikia malengo iliyokuwa ikiyafuatilia huko.
Kundi la Taliban lilichukua utawala wa Afghanistan mwezi Agosti uliopita baada ya serikali ya Rais Ashraf Ghani kusambaratika na rais huyo kulazimika kuikimbia nchi.